Sunday, September 12, 2010

Mwandishi Raymon Owaman wa RFA na Stav TV augua gafla!

Mwandishi huyo pichani juu aliugua gafla nyumbani kwake maeneo ya Kashabo na kukimbizwa katika hospitali ya Mkoa Kagera jana jumamosi na hadi sasa amelazwa hapo.

Taarifa kutoka kwa ndugu zake ni kuwa ugonjwa unaomsumbua mwandishi huyo bado haujajulikana na kwamba alianguka na kupoteza fahamu

tutawajuza maendeleo ya mchapakazi huyo.

imetolewa na Chama cha waandishi wa Habari Mkoani Kagera(KPC)

Tuesday, September 7, 2010

Huyu 'Muhuni" kwenye msafara wa Kikwete analipwa na nani

Na Antony Mayunga

NDEGE wa aina moja huruka kwa pamoja ,ni msemo wa wahenga wetu waliotutangulia,wakimaanisha watu wa itikadi moja hufanya mambo yao kwa pamoja.

Lakini msemo huo unakuwa kinyume kwa viongozi na wanachama wa baadhi ya vyama vya siasa kutokana na kampeni za uchaguzi mkuu unaoendelea kutawaliwa na vibweka vingi .

Miongoni mwao ni kauli ya iliyotolewa na Katibu wa CCM Taifa Yusuph Makamba kuhusiana taarifa kuwa kuna baadhi ya waandishi wa Habari walizuiwa kushiriki katika msafara wa Mgombea urais kupitia CCM

Makamba alikaririwa na vyombo vya Habari akidai kuwa mtu aliyefanya hivyo ni mhuni mmoja bila kumtaja jina.

“Huyo si uamuzi wa Chama ,ili uwe wa chama lazima uafikiwe na kamati kuu,Nec au uamzi afanye Katibu mkuu,vikao hivi havikufanyika kokote na mimi
katibu mkuu sijaagiza mtu awafukuze waandishi,fuatilia vizuri habari yako utagundua kuwa yupo mhuni amekosana nao akawafukuza,”mwisho wa kumnukuu Makamba wakati akihojiwa na gazeti la kila siku la Mwananchi.

Mimi nikiwa Mwandishi wa Habari kauli hiyo inanipa mashaka juu ya umakini wa chama hicho kikongwe
kuwa na ‘mhuni’ mmoja katika timu yao ya kampeini ambaye anaweza kuamua kuwafukuza waandishi harafu wakaishia kumkandia huku akiendelea na uratibu.

Kwa mjibu wa kamusi mhuni ni Mwanamme ambaye hajaoa,kapera,mseja,mtu asiyekuwa na mahali maalum pa kuishi,mwizi ,mvunjaji
sheria,mnyang’anyi,mchopozi.

Kama maana ni hiyo Makamba anataka kuwaambia wanachama wake kuwa wamekosa watu makini mpaka wakachukua watu wa namna hiyo.


Anataka watanzania waamini kuwa Mgombea Urais wa CCM katika timu ya kampeini ya mgombea huyo kuna baadhi ya watu ambao ni wavunjaji wa sheria,wasiojulikana makazi yao.

Hivi kweli mhuni ambaye hajulikani anawezaje kupewa jukumu kubwa kama hilo na akaharibu wakaishia kudai ni mhuni mmoja bila kuchukua hatua,hii si ni danganya toto?
Kama ni kweli ‘mhuni’ huyo aliwafukuza waandishi kwenye msafara wa Kikwete ataachwa aendelee na kuratibu kazi za wasiokuwa wahuni, tutaraji nini.

Hivi watazinduka siku akimfukuza kiongozi wa CCM kwenye msafara ,na ni nani anamlipa mhuni huyo kwa kuzunguka na msafara huo?.

Inawezekanaje mhuni akapewa kitengo kizito cha kuamua mwandishi gani ashiriki msafara na nani abaki.

Je kwa kauli hiyo inamaanisha nani alimchagua na alipewaje nafasi hiyo ili hali wakijuakuwa
ni mhuni.

Nadhani ipo haja ya kutueleza jina kamili la mhuni huyo kwani Makamba alidhani kwa kusema hivyo kunatosha kuwaridhisha wananchi kuwa chama kimesikitishwa na kitendo hicho haramu.

Kwa kweli hizo ni porojo ambazo kwa zama hizi hazitakiwi kuvumiliwa maana kwa kufanya hivyo ,inatia shaka juu ya utendaji wa chama hicho kinachojigamba kila kukicha kuwa ni makini .

Maana huwezi kupata chama makini bila kuwa na watendaji makini,kwanza.

Kwanini uhuru wa waandishi uingiliwe, na kwa maslahi ya nani.

Katika katiba ya Jamhuriya Muungano ya mwaka 1977 ibara ya18(d),kifungu hiki kinampa haki mwananchi ya kupewa taarifa mbalimbali muhimu kuhusu maisha na shughuli za wananchi na pia kuhusu masuala
muhimu kwa jamii na watu wa kufanya kazi hii ni waandishi wa Habari kama waliofukuzwa.

Hivyo kwa chama makini kukaa kimya kwa mtu kuvunja katiba ibara hiyo kwa kifungu (b)na (c)kwa waandishi wa habari,inawapa mashaka watanzania wanaotaraji kufanya maamzi yao sahihi oktoba 31 .

Maana kwa kuwazuia waandishi kulikuwa na agenda ya siri isiyotakiwa kujulishwa jamii,ambayo inahitaji taarifa nani anafanya nini na wapi ,na anamkakati wa kuwafanyia nini watanzania.

Hivyo kumwachia “mhuni” rungu ya kubagua waandishi katika kampeini za Kikwete ni hatari sana.

Aidha waandishi wanaoandamana na wagombea waanchu ushabiki,kuvaa sare za vyama kwani hivyo ni kinyume na maadili ya taaluma.

Kwa kuacha hulka hizo watatenda kazi zao wakiwa huru,bila kuvalishwa nguo za chama ,na hayo ndiyo matarajio ya jamii kwa kipindi hiki ambacho
wanahitaji uchambuzi wa kina wa sera ,ilani na mikakati ya vyama vyote na wala si ushabiki.

Mwandishi anapatikana kwa simu no 0787239480.

Makala hii imetolewa kwenye gazeti Malengo Yetu Toleo la leo septemba 7,2010

Mapungufu kwa wagombea wote haya hapa !


Na Mwandishi Wetu.




Harakati za kampeni zikiwa zimepamba moto kwa wagombea wa nafasi za Urais,Ubunge na Udiwani tayari kumejitokeza mapungufu makubwa ambayo iwapo hayatarekebishwa yanaweza kuathiri mantiki nzima ya mchakato wa uchaguzi Mkuu.




Aidha imebainika kuwa hakuna chombo chochote kinachoratibu kampeini za wagombea kubaini kama wanayoyafanya kwenye kampeini zao ni sawa au wafanye marekebisho.




Uchunguzi wa gazeti hili tangu kuanza rasmi kwa kampeini hizo August 20 mwaka huu umebaini kuwa wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge wanafanya kampeini ambazo hazitoi nafasi kwa wapiga kura kuwapima.




Hivyo hivyo wagombea nafasi za Urais wakiwemo Mutamwega Mutahywa(TLP),Hashimu Rungwe (NCCR-Mageuzi),Ibrahimu Lipumba,Willbroad Slaa(CHADEMA) na Jakaya Kikwete(CCM) ambao tayari wamezindua kampeini zao nao wamekumbwa na ‘ugonjwa huo’.




Kwa mjibu wa Uchunguzi huo ni kuwa kati ya wagombea hao hakuna hata mmoja anayetoa fursa za kuulizwa maswali au kuwataka wasikilizaji kupata ufafanuzi wa jambo lolote.




Imebanika kuwa wagombea wote wamekuwa wakihutubia tu na baada ya mkutano kuondoka huku wakiacha maswali mengi kwa wapiga kura ambao hukosa fursa ya kujua hasa mgombea alichosema .Na wanaotaka kupata ufafanuzi wa jambo lililosemwa huachwa njia panda




Mathalan,mgombea anasema kuwa iwapo atachaguliwa atahakikisha nchi inaondokana na umaskini kwa muda wa siku 100 lakini hatoi nafasi kwa wananchi kuuliza jambo juu ya hoja zake hizo.




Wapiga kura waliohojiwa walisema kuwa hawaoni haja ya kwenda kwenye mikutano ya kampeini kwani inakuwa kama wanapata hotuba zilizorekodiwa kupitia kwenye redio au Television.




Uchunguzi umebaini kuwa hata katika ratiba zao hakuna kipengele cha maswali bali kuna muda wa wagombea kuongea na wananchi na siyo kueleza sera zao.




“Wote hawataki tuwaulize maswali na wanatoi ahadi ambazo hata hazitekelezeki na wengine walishindwa kutekeleza kwa kipindi cha nyuma lakini kwa kuwa hawatoa fursa ya maswali wanatulisha sera zao tu na kuondoka”Alisema Bw Theresphory Maiko mkazi wa Rwamishenye Bukoba mjini.




Akihojiwa na gazeti hili Mwanasheria wa kituo cha Sheria na Haki za binadamu(LHRC) cha Jijini Dar Es Salaam Pasience Mlowe ni kuwa hayo ni mapungufu makubwa kikatiba.




Mlowe anasema kuwa iwapo wananchi hawapati fursa hivyo ni vigumu kuwapima wagombea kwani na kwamba hii inaweza kuathiri mchakato wa kampeini kwao wengine wanaweza kudhani ndiyo utaratibu kumbe siyo.




“Ni haki ya wananchi kikatiba,wananchi kuhoji mgombea juu ya jambo lolote alilosema kwenye mkutano au kupata ufafanuzi wa jambo hilo na kinyume chake ni makosa hivyo ni wajibu wa wananchi kudai haki hiyo” Alisema.




Kwa upande wake Rais wa Shirika la People Organization Transparency Agency(POTA) Idrisa Masalu ni kuwa hotuba zinazotolewa katika mikutano ya hadhara ni lazima wananchi wapate fursa ya kuuliza maswali.




“Hii ni hasara kwa wagombea na wapiga kura kwani bila maswali,mgombea atapataje uhakika kama wapiga kura wameelewa na mpiga kura atajuaje kama anachosema mgombea ni sahihi”Alisema Masalu na kuongeza




“Sera siyo biblia,ni lazima mgombea aulizwe na ukiona anayekataa kufanya hivyo ujue hajiamini na anaogopa kuumbuka na kwa lugha nyepesi anapiga propanganda tu aelezi sera”.




Mbali na kasoro za kutokubali kuulizwa maswali pia imeibuka tabia ya baadhi ya wagombea kutoa ahadi zisizo tekelezeka na baadhi yao kufanya kampeini za matusi badala ya kueleza sera zao.




Mathalan,katika mikutano ya kampeini za CHADEMA,CUF na CCM ambazo zimefanyika katika uwanja wa mafumbo(CHADEMA),uwanja wa Uhuru(CUF na CCM) wagombea wamebanika kujadili mienendo ya wagombea wa vyama vingine tofauti na kueleza sera zao.




Wagombea hao wanatumia dakika 28 kati ya 30 walizopewa kutukana,kueleza sifa mbaya za wagombea wa vyama vingine,kutoa taarifa zisizo na udhibitisho juu ya wenzao,uzuri wa chama chao na dakika mbili au tatu ndizo wanazotumia kueleza sera na nini watawafanyia wananchi iwapo watachaguliwa.




Aidha imegundulika pia kwenye ajenda za kujadili kwenye mikutano hiyo ya vyama zimo ajenda za kujadili wagombea wa vyama tofauti na vyao




Baadhi ya wanachama wa vyama vya siasa vya CHADEMA,CUF na CCM walihojiwa juu ya kasoro hizo katika kampeini wengi walionekana kutojua faida wala madhara yake huku wengine wakionekana kuwa nas jazba kwa kudai kuwa muuliza swali ametumwa na wapinzani wao.




Hakuna kiongozi yoyote wa Vyama hivyo ngazi ya mkoa aliyekuwa tayari kutoa ufafanuzi juu ya kasoro hizo kwa madai wao wanajua mbinu za kutumia wakati wa kampeini.




Aidha Jeshi la polisi nchini limenoa askari wake na kuwapatia mavazi na vifaa vipya kama wanavyoonekana pichani mbele mahususi kwa ajili ya kudhibiti vurugu wakati wa mchakato wa uchaguzi kwa nchi nzima


Hii ndiyo habari kubwa kwa gazeti Malengo Yetu Toleo la leo Septemba 7,2010